Shirika la Habari la Kimataifa la Ahlul-Bayt (a.s) -ABNA-: Je, Qur’ani Tukufu imewahimiza wanaume wote kufanya ndoa ya muda, au ndoa ya muda ni suluhisho kwa hali maalumu za mtu binafsi na kijamii?.
Jibu:
“Ndoa ya muda” ni aina ya ndoa inayofungwa kwa muda maalumu na uliobainishwa (baina ya watu wawili - Yaani: Baina ya Mwanaume na Mwanamke wanaofunga ndoa hiyo), sio ndoa ya kudumu na ya milele.
Katika mahusiano haya ya ndoa ya muda, kubainisha kwa usahihi muda wa ndoa na kiwango cha mahari (kujulikana) ni lazima, na mwanamke katika kipindi hicho hana haki ya kuolewa na mtu mwingine. Tofauti na ndoa ya kudumu inayomalizika kwa talaka, katika ndoa ya muda kutengana hutokea pindi muda ulioainishwa (uliowekwa) na wana ndoa hao wawili unapomalizika au mwanaume anaweza kusamehe muda uliobaki.
Iwapo mmoja wa pande mbili atafariki katika muda wa ndoa, hakuna yeyote atakayemrithi mwenzake; pia tofauti na ndoa ya kudumu, kulipa nafaka kutoka kwa mume kwa mke katika ndoa ya muda si wajibu. Lakini ikiwa mtoto atazaliwa kutokana na ndoa hii, kwa mtazamo wa kisheria hana tofauti yoyote na watoto wa ndoa ya kudumu, na kama wao atawarithi wazazi wake na nafaka yake ni wajibu kwa baba yake.
Baada ya kumalizika kwa muda wa ndoa au kusamehewa muda na mwanaume, ikiwa mahusiano ya kindoa yamefanyika, mwanamke anatakiwa kushika eda, na baada ya hapo ataruhusiwa kuolewa tena.
Ndoa ya Muda katika Qur’ani
Aya ya 24 ya Surah “An-Nisā’” katika Qur’ani Tukufu inahusu ndoa ya muda:
“…Basi kwa wanawake mliostamtii, wapeni mahari yao kama faradhi…” (1).
Maksud ya “istimta’” katika aya hii ni “ndoa ya muda”; kwa hiyo kwa mujibu wa aya hii, ndoa ya muda ni halali (2). Hoja muhimu kuhusu aya hii ni kwamba ingawa inajumuisha watu wote na hali zote na kwa istilahi haikubainishwa wala kuwekewa mipaka kwa hali au watu maalumu, iko tu katika kubainisha hukumu ya mahari katika aina hii ya ndoa na kusisitiza ulazima wa kuilipa; kwa hiyo si katika aya hii wala katika aya nyingine yoyote kuna kuonekana himizo la kufanya ndoa ya muda.
Ndoa ya Muda katika Riwaya
Uchunguzi wa riwaya unaonyesha kuwa Waislamu wa mwanzo wa Uislamu katika mazingira kama safari ambapo hawakuwa na ufikivu kwa wake zao, walielekea katika aina hii ya ndoa (3); kwa mfano, imenukuliwa kutoka kwa Abdullah bin Mas‘ud sahaba kwamba ndoa ya muda iliruhusiwa wakati Waislamu walipotoka Madina kwa ajili ya vita na walikuwa katika taabu ya kukosa wake (4). Kwa mujibu wa riwaya nyingine, Mtume aliruhusu jambo hili wakati walipokuwa wamekwenda kutoka Madina kwenda Makka kwa ajili ya Umra (5). Riwaya nyingine pia inasema iliruhusiwa wakati wa kufunguliwa kwa Makka (6).
Katika baadhi ya riwaya za Ahlul-Bayt (a.s) pia tunaona kwamba waliwaambia baadhi ya masahaba wao waliokuwa wameoa na walikuwa na ufikivu kwa wake zao: “Wewe una nini na Mut’a, hali ya kuwa Mwenyezi Mungu amekutosheleza kutokana nayo?” (7).
Katika riwaya nyingine kutoka kwa Imam Mūsā al-Kāẓim (a.s) imekuja hivi: “Mut’a ni halali na mubaha kabisa kwa yule ambaye Mwenyezi Mungu hakumtosheleza kwa ndoa (ya kudumu), basi ajisitiri kwa Mut’a; na ikiwa amejiweza kutokana nayo kwa ndoa (ya kudumu), basi ni mubaha kwake pale anapokuwa mbali naye (mkewe)” (8). Kwa msingi wa riwaya hizi, wafasiri wengi wa Kishia katika kubainisha sababu ya kuhalalishwa kwa ndoa ya muda katika Uislamu wameashiria mambo kama kutokuwepo kwa mazingira ya ndoa ya kudumu, safari ndefu na majukumu ya watu waliooa na kadhalika (9).
Kwa mujibu wa riwaya za Ahlul-Bayt (a.s), katika aina hii ya ndoa haipaswi kuelekea kwa wasichana mabikira (10), na pia wanawake waovu, na haipaswi kusisitiza juu ya jambo hili hadi kusababisha kupuuza wake wa kudumu na kuwakasirisha (11).
Hitimisho
Asili ya uhalali wa ndoa ya muda imebainishwa na Mtume Muhammad (s.a.w.w), na Mwenyezi Mungu katika aya ya 24 ya Surah An-Nisā’ huku akithibitisha uhalali wake, amebainisha mojawapo ya hukumu zake. Qur’ani iko tu katika kubainisha hukumu ya kisheria na aya ya Mut’a haina aina yoyote ya himizo kuhusu jambo hili. Kwa mujibu wa ripoti za kihistoria, Mtume wa Mwenyezi Mungu (s.a.w.w) wakati walipokuwa safarini kwa vita au Umra na masahaba hawakuwa na ufikivu kwa wake zao, waliiruhusu ndoa ya muda; hata hivyo, kama ilivyothibitika katika misingi ya fiqhi, sababu ya kutolewa kwa hukumu haiweki mipaka juu yake;
Kwa hiyo, ndoa ya muda kwa namna ya jumla katika safari na pia isiyo safari, kwa watu wasiooa na pia waliooa, kwa waliooa wanaoweza kufikia wake zao au wasioweza, iwe kuna uwezekano wa ndoa ya kudumu au la, ni halali; lakini kwa mujibu wa riwaya za Maimamu waongofu (a.s), katika ndoa ya muda haipaswi kuelekea kwa wasichana mabikira na pia wanawake waovu, na wanaume waliooa wanaoweza kufikia wake zao wamehesabiwa kuwa hawana haja nayo; kwa hiyo wameombwa wasifanye jambo hili hadi lisababishe kupuuza wake wao wa kudumu na kuwahuzunisha.
Rejea
-
Surah An-Nisā’, Aya ya 24.
-
ʿAlī bin Ibrāhīm al-Qummī, Tafsīr al-Qummī, Qum: Dār al-Kitāb, 1404 H, Juz. 1, uk. 136.
-
ʿAbd al-Raḥmān bin Muḥammad Ibn Abī Ḥātim, Tafsīr al-Qur’ān al-ʿAẓīm, Riyadh: Maktabat Nizār Muṣṭafā al-Bāz, 1419 H, Juz. 3, uk. 919.
-
Aḥmad al-Ṭabarānī, al-Tafsīr al-Kabīr, Jordan: Dār al-Kitāb al-Thaqāfī, 2008, Juz. 2, uk. 218.
-
Aḥmad al-Thaʿlabī, Tafsīr al-Thaʿlabī, Beirut: Dār Iḥyā’ al-Turāth al-ʿArabī, 1422 H, Juz. 3, uk. 287.
-
Yaʿqūb Jaʿfarī, Tafsīr Kawthar, Qum: Hijrat, 1398 Sh, Juz. 2, uk. 400–401.
-
Aḥmad bin Muḥammad bin ʿĪsā al-Ashʿarī al-Qummī, al-Nawādir, Qum: Madrasat al-Imām al-Mahdī (a.f), 1408 H, uk. 87.
-
Muḥammad bin Yaʿqūb al-Kulaynī, al-Kāfī, Tehran: Dār al-Kutub al-Islāmiyyah, 1407 H, Juz. 5, uk. 452–453.
-
Nāṣir Makārim Shīrāzī na wenzake, Tafsīr Namūnah, Tehran: Dār al-Kutub al-Islāmiyyah, 1371 Sh, Juz. 3, uk. 342; Muḥsin Qarā’atī, Tafsīr Nūr, Tehran: Markaz-e Farhangī Dars-hā’ī az Qur’ān, 1388 Sh, Juz. 2, uk. 45; Yaʿqūb Jaʿfarī, Tafsīr Kawthar, Juz. 2, uk. 408; Muḥammad ʿAlī Riḍā’ī Iṣfahānī, Tafsīr Qur’ān Mehr, Qum: Pazhūhesh-hā-ye Tafsīr wa ʿUlūm al-Qur’ān, 1387 Sh, Juz. 4, uk. 94; ʿAlī Akbar Qurashī Banābī, Tafsīr Aḥsan al-Ḥadīth, Tehran: Bunyād Biʿthat, 1375 Sh, Juz. 2, uk. 339.
-
Aḥmad bin Muḥammad bin ʿĪsā al-Ashʿarī al-Qummī, al-Nawādir, uk. 86.
-
Muḥammad bin Yaʿqūb al-Kulaynī, al-Kāfī, Juz. 5, uk. 454.
Your Comment